MKUU wa Mkoa wa Kagera, Kanali Mstaafu Fabian Massawe, amesitisha likizo zote kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri hadi ujenzi wa majengo ya maabara utakapokamilika.
Mbali na kusitisha kwa likizo hizo, Massawe ametishia kuwawajibisha viongozi watakaoshindwa kutimiza na kukamilisha ujenzi wa maabara katika shule zote za kata za mkoa huo kwa muda uliopangwa.
Kanali Massawe alitoa agizo hilo jana alipozungumza na waandishi wa habari ofisini kmwake, kuhusiana na mkoa kukabiliwa na upungufu wa majengo 457 ya maabara za sayansi kwa wanafunzi wa shule za sekondari za Kata.
Alisema ujenzi wa majengo hayo lazima ukamilike kabla ya Desemba, mwaka huu kama alivyoagiza Rais Jakaya Kikwete.
Alisema kukamilika kwa majengo hayo kutaleta manufaa kwa watoto walioko shuleni sasa na vizazi vijavyo.
Alisema mkoa huo pia bado unakabiliwa na upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi, na kwamba wale waliopo ni wa masomo ya sayansi sanaa wanaozalisha wanasiasa wengi kuliko wanasayansi.
Alisema nchi yoyote haiwezi kupata maendeleo kwa kuwa na wanasiasa bila wanasayansi, hivyo alisema wananchi wa mkoa wa Kagera wataendelea kukusanya vifaa vya ujenzi kujenga maabara hizo.
NA JESCA WILLY
No comments:
Post a Comment